Subscribe:

search

.

Friday 31 August 2012

GAVANA AZINDUA MFUKO WA KUNUNUA DHAMANA

GAVANA wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndullu akiongea na waandishi wa habari  jijini Dar es salaam kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo mfumo wa mawakala wa Benki hiyo wa kununua dhamana za Serikali na hati fungani kwa njia ya mtandano(online) kwenye mnada na hivyo kupunguza ule utaratibu wa dhamana wa kupeleka karatasi katika Benki ili kupata huduma hiyo.

Monday 27 August 2012

UJUMBE WA KIPANYA LEO


HUU HAPA MSIMAMO WA MNYIKA JUU YA VURUGU ZILIZOTOKEA MOROGORO

Niliwahi kutahadharisha baada ya tukio la Dkt Stephen Ulimboka kuwa serikali imeanza kutumia mbinu haramu kudhibiti fikra mbadala, CCM imeanza kuongoza serikali kiimla na ipo siku umma utafikia hatua ya kukiona kama chama cha mauaji. Raia watatu wasio na hatia wamefyatuliwa risasi na mmoja amefariki. Haya yamefanyika kwenye maandamano ya amani ya wananchi kuwapokea viongozi wa CHADEMA kuelekea kwenye mkutano. Vurugu zimeanzishwa na polisi kwa mujibu wa mashuhuda wa ushahidi wa video. Vyanzo vyangu vinaniambia sasa wameagiza gari tatu za FFU na gari za kuwasha toka Dar Es Salaam. Tuombe MUNGU wasiamue kuvuruga mkutano wa hadhara ambao wananchi wamekusanyika kwa wingi hivi sasa. States captured by grand corruption of the ruling party cronies for so many years resorts to bullets as a way of stopping M4C through the ballot. Maisha ya wachache yako mashakani lakini si mabadiliko kwa maslahi ya wengi.

John John MNYIKA,
27 Agosti, 2012

WAKULIMA WA MPUNGA KATAVI WANUSURIWA

 
Waziri MKUU Mizengo Pinda
Magreth Munisi
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewataka wakulima wa mpunga nchini kuanza kujipanga kuuza mchele nje ya nchi.
Pinda alisema hayo juzi wakati akikagua kazi ya kuweka mitambo ya kinu cha kukoboa mpunga katika kata ya Mwamapuli na Majimoto wilayani Mlele mkoani Katavi, na ujenzi wa madaraja ya mto Msadya na mto Kavuo.

Aliendelea kusema kuwa kulingana na mahitaji yatakayokuwepo, wakulima hao kama watajipanga vizuri wanaweza kuuza mchele watakaouzalisha hadi katika nchi za Burundi na Rwanda ambako soko la uhakika lipo.

“Kwa mahitaji yatakayokuwepo, na kama wakulima watajipanga vizuri wanaweza kuuza mchele mpaka nchi za Rwanda na Burundi,” alisema Pinda kwenye taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na ofisi yake.

Aliendelea kufafanua kuwa kukamilika kwa mradi huo kutawasaidia wakulima kuuza mchele badala ya kuuza mpunga, ndipo alipoelekea Mwampuli kukagua kinu hicho kilichonunuliwa kwa fedha za Halimashauri kwa lengo la kuwasaidia wananchi wa kata hizo

Kwa upande mwingine, diwani wa kata hiyo, Emmanuel Mponda alimweleza Waziri Mkuu kuwa kinu hicho kina uwezo wa kukuboa tani 300 kwa siku kikiendeshwa kwa saa nane kutwa nzima.

Diwani huyo alieleza kuwa kinu hicho kina uwezo wa kuchambua mchele na kuupanga katika madaraja manne tofauti na kuufungasha kwa madaraja hayo, na kinatarajiwa kuanza kazi Septemba mara jenereta litakapokamlika kuunganishwa.
“Mchele ukishakobolewa, unapangwa katika madaraja A, B, C, na daraja D zinakuwa ni chenga ambazo zitauzwa peke yake kwa ajili ya wauza vitumbua. Kinu hiki pia kina uwezo wa kutenganisha pumba kwa ajili ya mifugo na kuzipaki katika sehemu ya peke yake bila kuingiliana na uzalishaji wa mchele,” alisema Mponda.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda Vijijini, Wilbroad Mayala alisema kinu hicho kimegharimu Sh96 milioni wakati jenereta la kuendesha kinu hicho lenye uwezo wa kuzalisha kilowati 120, limenunuliwa kwa sh86 milioni.
Chanzo:mwananchi.co.tz

HII NI TASWIRA YA NAMNA WATU WALIVYOJITOKEZA KATIKA MKUTANO WA M4C MOROGORO

PICHA MBILI ZA KIJANA ANAEDAIWA KUUWAWA NA POLISI HUKO MOROGORO KATIKA MAANDAMANO YA CHADEMA





Hizi ni baadhi ya picha za kijana anaedaiwa kuuwawa katika maandamano ya CHADEMA huko Morogoro.

NAPE AKATAA KUIOMBA RADHI CHADEMA



Akataa kuomba radhi, asema tuhuma atazithibitisha mahakamani, Amtaka Dk. Slaa kuandaa bilioni 3 na shilingi moja. Ni kwa kudai CCM inaingiza silaha nchini.

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye amewataka Chadema kwenda mahakamani haraka badala ya kusubiri kuombwa radhi kama walivyotaka ili kusafishwa dhidi ya madai ya chama chao kupewa mabilioni ya fedha na mataifa tajiri.

Aidha amemtaka Katibu Mkuu wa chama hicho Dk. Wilbrod Slaa kuiomba radhi CCM la sivyo itamburuza mahakamani kudai fidia ya sh. bilioni 3 na shilingi moja, kwa kuituhumu uongo kwamba imeingiza silaha kutoka nje ya nchi tena bila kulipia ushuru.

Nape alisema hayo leo Agosti 27, 2012, kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, uliofanyika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, mtaa wa Lumumba mjini Dar es Salaam.

"Bila shaka mmesikia jana Chadema wakinitaka niombe radhi au wananipeleka mahakamani kudai fidia ya sh. bilioni 3, kwa madai eti nimesema Chama hicho kinapata mabilioni ya fedha kutoka kwa mataifa tajiri. Mkubwa hatishiwi nyau, nawataka waende haraka mahakamani wala wasisubiri hizo siku saba", alisema Nape.

Alisema, CCM inao ushahidi wa kutosha kuhusu madai aliyotoa Nape dhidi ya Chadema na kwamba huyo tayari kutoa uthibitisho huo mahakamani badala ya kuomba radhi.

"Nadhani wakienda mahakani itapendeza zaidi maana huko ndiko pazuri kutoa uthibitisho kuhusu tuliyosema, na ninawahakikishieni tukishathibitisha na Msajili wa Vyama akaupata uthibitisho huo chama chao kinafutwa", alisema.

Kuhusu CCM kumburuza Dk. Slaa mahakamani, Nape alisema, ameshawaagiza wanasheria wa Chama, kuandaa barua ya kusudio la mashitaka hayo, na Dk. Slaa atapelekewa ili aamue kama ataomba radhi au atakuwa tayari kwenda mahakamani.

"Wakati wanakwenda mahakamani, Chadema wamwambie babu yao ajiandae kuomba radhi au kuburuzwa mahakamani kuilipa CCM fidia ya sh. bilioni 3 na shilingi moja kwa kuizushia CCM uongo kwamba inaingiza silaha nchini tena", alisema Nape.

Bashir Nkoromo
Blogger & Senior Photojournalist
Uhuru Publications Ltd,
Publishers of Uhuru, Mzalendo and Burudani tabloids
Cell; +255 712 498008, +255 789 498008, +255 773 600007 +255 756 646131
E-mail: nkoromo@gmail.com, bnkoromo@yahoo.com. 
P O Box 9221, Dar es Salaam.Tanzania, East Africa

POLISI WAWAPIGA MABOMU WAFUASI WA CHADEMA MOROGORO



Wafuasi wa chama cha demokrasia na maendeleo chadema
 Askari waliokuwa katika eneo la tukio kabla ya kuanza kwa maandamano hayo
 Moshi wa mabomu yaliolipuliwa kutawanya maandamano ya chadema leo mjini morogoro


 Gari  la chadema lililokuwa likiongoza maandamano hayo

HUYU HAPA NI MWENYEKITI WA CHADEMA JIJINI LONDON


ANAEONEKANA KWENYE PICHA NI CHRIS LUKOSI MWENYEKITI WA CHADEMA JIJINI LONDON. HAPO ALIKUWA ANAJIANDAA KUELEKEA KWENYE MKUTANO WA CHADEMA HUKO READING.

CHADEMA WAPATA WANACHAMA WAPYA 3,500 MKOANI MARA

 Mwenyekiti wa Baraza la Vijana taifa wa Chadema(BAVICHA),John Hecheakigawa kadi mpya kwa wanachama wapya wa chadema
  Mwenyekiti wa Baraza la Vijana taifa wa Chadema(BAVICHA),John Heche akionyesha baadhi ya kadi za wananchama wa CCM Wa
-- 
OPARESHENI maalumu ya ‘Vua gamba vaa Gwanda’ inayoongozwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imeitikisa Wilaya ya Tarime mkoani Mara, baada ya zaidi ya wanachama 3,500 wakiwemo viongozi wa CCM kujiunga na CHADEMA wilayani hapa.
Mbali na idadi hiyo ya watu kujiunga na CHADEMA, pia wananchi wengi wamegombania kadi za chama hicho kama njugu, ikiwa ni lengo la kutaka kujiunga na harakati za vuguvugu la kutaka kuleta mabadiliko ya kisiasa hapa nchini kuelekea uchaguzi wa Serikali za mitaa mwaka 2014, na hatimaye uchaguzi mkuu mwaka 2015.
Wanachama hao wakiwemo viongozi wa CCM wamejiunga na CHADEMA wakati wa mkutano wa hadhara wa chama hicho, uliofanyika mjini Sirari kisha kuhutubiwa na mwenyekiti wa Baraza la Vijana taifa wa chama hicho (BAVICHA), John Heche.

Miongoni mwa viongozi wa CCM waliorudisha kadi kisha kukabidhiwa kadi za CHADEMA mkutanoni hapo, ni pamoja na mjumbe wa Serikali ya Kijiji cha Sirari, Masha Vincent ambapo mke wake pia Veronika Masha alirudisha kadi ya CCM kisha kujiunga na CHADEMA.

Akizungumza kwa niaba ya wanachama wengine wapya waliojiunga na chama hicho kikuu cha upinzani nchini mara baada ya kukabidhiwa kadi za Chadema, Masha alisema wamechukuwa uamuzi huo baada ya kuchoshwa na kile alichodai majungu, fitina na uhasama unaofanywa na baadhi ya viongozi wa CCM wilayani hapa.

Alisema, enzi za CCM zinaonekana kuelekea kuisha, hivyo kujiunga kwao na CHADEMA ni kuongeza vuguvugu la mabadiliko, na kuwaomba vijana kufanya maamuzi ya dhati katika kuleta mabadiliko ya kisiasa, kijamii na kiuchumi.

“Mimi nimeamua kuondoka rasmi CCM. Maana yupo kiongozi mmoja hapa Sirari alikuwa anatusakama baada ya kumpinga mambo yake. Sasa tupo kwenye chama makini na chenye mtazamo mpana katika maendeleo ya nchi hii”, alisema Masha kisha kushangiliwa na umati mkubwa wa watu.

Awali, mwenyekiti wa Bavicha taifa, John Heche aliwaomba Watanzania kutumia kura zao vizuri uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2014 pamoja na uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika nchini mwaka 2015 kwa kuipigia kura CHADEMA ili ishike dola na kuleta mabadiliko ya kweli katika maendeleo ya wananchi.

Alisema, CHADEMA imedhamiria kuleta ukombozi mpya kwa wananchi wa taifa hili, na kwamba iwapo Watanzania wataiwezesha kuingia madarakani mwaka 2015, itahakikisha serikali yake inatumia vizuri rasilimali za nchi kwa faida ya Watanzania wenyewe na si wawekezaji.

Aidha, akiwa katika mkutano wa hadhara kule Muriba Tarime jana, Heche alilaani vikali mauji ya vijana yanayodaiwa kufanywa na baadhi ya askari polisi katika mgodi wa dhahabu wa Nyamongo uliopo wilayani hapa, na kusema upo uwezekano wa kuishtaki serikali ya Tanzania katika mahakama ya Kimataifa ya makosa ya uhalifu (ICC), kuhusiana na mauaji hayo.

Alisema, CHADEMA haiwezi kuendelea kuona Watanzania wanauawa kama wanyama katika wilaya hiyo, hivyo ikibidi ipo siku serikali italazimika kwenda kujibu mashtaka kwenye mahakama hiyo ya ICC kuhusiana na unyama inaowafanyia wananchi wake kwa kuruhusu jeshi lake la polisi kutumia mtutu kuwaua raia mgodini hapo.

“Hatuwezi kukubali vijana wetu, Watanzania wenzetu, wakurya wenzetu waendelee kuuawa kwa kupigwa risasi na polisi katika mgodi wa Nyamongo. Ipo siku serikali ikibidi itashtakiwa ICC kutokana na mauaji ya wananchi wetu”, alisema mwenyekiti huyo wa Bavicha taifa, Heche.

Alisema, mgodi wa Nyamongo kama ungelitumiwa vizuri na Serikali ya CCM ingelisaidia kupeleka maendeleo ya elimu, barabara, maji safi na salama ya kunywa, hospitali pamoja na mawasiliano, lakini kwa sasa madini hayo yanatumika kuwanufaisha raia wa nje ya nchi.
Hata hivyo, aliituhumu Serikali ya CCM kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete kwamba utawala huo umekuwa ombaomba namba moja kwa misaada huko Ulaya, na kusema wakati mwingine Rais Kikwete huwa anapishana na ndege za wazungu zikiwa zimebeba madini, huku kiongozi huyo naye akitoka Ulaya kuomba vyandarua, jambo ambalo litaenda kudhibitiwa na CHADEMA itakapoingia Ikulu 2015.
Chanzo: Hakingowi.com

Sunday 26 August 2012

KAMATI KUU YA CCM YAWAPONGEZA BAADHI YA MAWAZIRI WAKE


Raymond Kaminyoge
KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (CC), imewapongeza mawaziri kwa kuchukua hatua dhidi ya watendaji wanaotuhumiwa kwa vitendo vya matumizi mabaya ya ofisi za umma wakiwamo wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na kuwataka waendelee na kasi hiyohiyo.
Pongezi hizo za Kamati Kuu zimetolewa baada ya kikao chake kilichofanyika Ijumaa iliyopita na zimekuja baada mawaziri kadhaa kuwachukulia hatua za kinidhamu baadhi ya watendaji walio chini ya wizara zao kwa tuhuma mbalimbali.
Mawaziri waliowachukulia hatua watendaji ni pamoja na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda.
Juzi, Kamati Kuu iliipongeza Serikali kwa kutekeleza maagizo yake ya kutaka ichukue hatua dhidi ya watendaji waliohusishwa katika ubadhilifu katika mashirika ya umma.
“Kamati Kuu inawapongeza mawaziri walioanza kutekeleza maagizo hayo kwani mwisho wa siku maisha bora kwa kila Mtanzania yatawezekana,” ilisema taarifa iliyotolewa jana na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye.
Kamati Kuu ilieleza katika taarifa yake kuwa ipo haja ya kuwachukulia hatua watendaji wakuu wa mashirika yaliyohusishwa na ubadhirifu mbalimbali na kwamba kitendo hicho cha mawaziri hao ni kutekeleza agizo lake.
Mei 17, mwaka huu, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Kigoda alimsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Charles Ekelege ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa zikimkabili.
Miongoni mwa tuhuma hizo ni pamoja na kuyapa zabuni kampuni hewa za ukaguzi wa magari kabla hayajaingia nchini.
Muda mfupi baadaye, Juni 5, mwaka huu, Dk Mwakyembe alimsimamisha kazi Kaimu Mtendaji Mkuu wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Paul Chizi kutokana na tuhuma mbalimbali.
Hivi karibuni, pia Dk Mwakyembe alisimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Ephraim Mgawe, wasaidizi wake wawili na Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Cassian Ng'amilo kupisha uchunguzi wa wizi wa vitu mbalimbali yakiwemo makontena 40 ya vitenge katika Bandari ya Dar es Salaam.
Pia aliwasimamisha kazi Meneja wa Kituo cha Mafuta ya Ndege Kurasini (Kurasini Oil Jet - KOJ), Meneja wa Kituo cha Mafuta JET na mhandisi wa mafuta wa kituo hicho, baada ya kubainika kuwepo kwa wizi wa mafuta.
Waziri Kagasheki kwa upande wake, alimfukuza kazi Mkurugenzi wa Wanyamapori, Obeid Mbanga kwa kashfa ya kusafirisha wanyama kwenda nje ya nchi.
Julai 14, mwaka huu, Bodi ya Tanesco ilimsimamisha kazi  Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo, William Mhando ikielezwa kuwa ni maelekezo ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Muhongo ili kupisha uchunguzi wa matumizi mabaya ya madaraka katika ofisi yake.
Mbali na kupongeza kazi hiyo, pia CC ilizungumzia mgogoro wa Tanzania na Malawi. Kuhusu hilo, Nape alisema Kamati Kuu imewatahadharisha wanasiasa na vyombo vya habari vinavyochochea vita na uhasama kati ya nchi hizo mbili.
“Kamati Kuu imetaka suala hilo kuiachia diplomasia ichukue mkondo wake na Serikali iushughulikie na kuumaliza mgogoro huo,” alisema Nape.
Pia, ilipokea taarifa ya maendeleo ya uchaguzi ndani ya chama na kusema imeridhishwa na maendeleo hayo ya uchaguzi na kuagiza kila kikao husika kihakikishe haki inatendeka hasa katika uchujaji wa majina
Chanzo:Mwananchi.co.tz

UJUMBE WA KIPANYA LEO


NAIL Armstrong BINADAMU WA KWANZA KUFIKA MWEZINI AFARIKI DUNIA



 Hussein Issa ,Mashirika
NAIL Armstrong linaweza lisiwe jina maarufu enzi hizi, lakini hilo ndilo jina lililoshika chati mwishoni mwa miaka ya 1960 kwani alikuwa binadamu wa kwanza kukanyaga mwezini.Hata hivyo gwiji huyo wa mambo ya anga , amefariki akiwa na umri wa miaka 82 akiacha rekodi yake hiyo iliyotikisa dunia.
Neil Armstrong alitua mwezini Julai  20, 1969 akiwa katika chombo kilichoitwa Apollo na kusema ''hiyo ilikuwa hatua ndogo ya binadamu, lakini mapinduzi makubwa kwa ubinadamu''.
Armstrong na mwanaanga mwenzake Buzz Aldrin walitumia saa mbili na nusu wakitembea juu ya mwezi .  Neil Armstrong na wanaanga wenzake watatu Novemba mwaka 2011, walitunukiwa tuzo ya Congressional Gold Medal ambayo ndiyo ya juu zaidi inayotolewa kwa raia nchini Marekani.  Armstrong amefariki  dunia jana katika hospitali ya Columbus jimboni Ohio ambako alifanyiwa upasuaji wa moyo mapema mwezi huu.
Kulingana na wasifu wa Armstrong ambao umechapishwa na Shirika la Anga la Marekani, NASA, mwanaanga huyo aliyezaliwa jimboni Ohio mwaka 1930, alisafiri kwa ndege kwa mara ya kwanza akiwa na miaka sita, na kupata leseni ya kuendesha ndege akiwa na miaka 16, hata kabla ya kujua kuendesha gari.  Alitumikia Jeshi la Marekani kama rubani wa ndege za kivita wakati wa vita vya Korea, na baadaye akajiunga na masomo ya sayansi ya anga.   Baadaye aliajiriwa kama rubani wa kuzifanyia ndege majaribio.

Neil Armstrong alijiunga na programu ya anga mwaka 1962, na kurusha chombo cha kwanza cha anga miaka minne baadaye.   Aliteuliwa kuwa kiongozi wa wanaanga walioshiriki katika safari ya Apollo, ambayo iliwafikisha wanadamu wa kwanza mwezini.

Hatua yake ya kwanza mwezini iliangaliwa na mamilioni ya watu duniani kwa njia ya televisheni.Baada ya kutangazwa kwa kifo cha mwanaanga huyo, Mkuu wa Shirika la Anga la Marekani, NASA, Charles Bolden ametuma salamu zake za rambirambi kwa familia ya Armstrong.Charles Bolden amesema wakati wowote kutakapokuwa na vitabu vya historia, jina la Neil Armstrong litaandikwa kwenye kurasa za vitabu hivyo.
Amesifia jinsi Neil Armstrong alivyoishi maisha ya unyenyekevu, na kusema kuwa mfano wake ni wa kuigwa.   Pia Rais Barack Obama  wa Marekani ametoa salamu za rambirambi zake, na kusema mwanaanga huyo ni miongoni mwa mashujaa wakubwa wa Marekani.Amesema Armstrong pamoja na wenzake 11 katika chombo cha Apollo, walibeba matarajio ya taifa zima la Marekani katika safari yao ya anga mwaka 1969.
''Waliionyesha dunia ari ya Marekani kuangalia mbali zaidi ya yale yanayofikirika, na kuthibitisha kuwa penye juhudi na maarifa, kila kitu kinawezekana,'' amesema Obama, na kuongeza kuwa ujumbe alioutoa Armstrong baada ya kukanyaga kwenye ardhi ya mwezini, ni mafanikio ya binadamu ambayo kamwe hayatasahaulika.
Katika tangazo lililotolewa na familia ya Armstrong kufuatia kifo chake, mwanasayansi huyo ametajwa kuwa shujaa wa Marekani, ambaye muda wote yeye alisisitiza kuwa alichokifanya kilikuwa wajibu wake kikazi.  Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Familia yake imesema kuwa kifo chake kimetokana na matatizo yaliyofuatia upasuaji wa moyo.
Familia ya Armstrong imesema kuwa mwanaanga huyo aliendelea kufuatilia maendeleo ya safari za anga, na kila alipofanya hivyo shauku yake ya ujana ilijitokeza tena.  Neil Armstrong alistaafu kutoka NASA mwaka 1971 na alifanya kazi kwenye bodi ya wakurugenzi.   Hakupenda kuwa mtu wa kujionyesha onyesha, isipokuwa mara chache tu kwenye kumbukumbu za safari ya kwanza mwezini, au akiunga mkono kuendelea kwa utafiti wa anga.

Familia yake imesema kuwa, ingawa Neil Armstrong alipenda kuishi maisha yake bila bugudha, alifurahia ujumbe wenye nia njema kutoka kila pembe ya dunia kuhusu yeye na wenzake

Chanzo:Mwananchi.co.tz

MNYIKA ADAI CHADEMA ITAMFIKISHA NAPE NNAUYE MAHAKAMANI IWAPO HATOKIOMBA RADHI CHADEMA ZAIDI INGIA HAPA





Mbunge wa Ubungo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Mnyika akizungumza na waandishi wa habari leo asubuhi. (Picha na Habari Mseto Blog)




Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeanza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Nape Nnauye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM kufuatia madai ya uzushi na uongo aliyoyatoa tarehe 12 Agosti 2012 kuwa anao ushahidi kwamba CHADEMA kimekuwa kikiwahadaa wananchi kwa kuwachangisha fedha huku kikipokea mabilioni ya fedha kutoka kwa wafadhili kutoka nje.


Izingatiwe kuwa matamshi yake yalitangazwa na vyombo vya habari vya kielekroniki ikiwemo vituo vya televisheni, radio na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii tarehe 12 Agosti 2012 na katika kurasa za mbele za magazeti mbalimbali tarehe 13 Agosti 2012.


Bodi ya Wadhamini wa CHADEMA iliagiza wanasheria wamwandikie barua ya kumtaka kukiomba radhi Chama Cha Demokrasia na Maendeleo kwa kutumia njia ile ile aliyotumia kufanya propaganda chafu za kuikashifu na kuifitisha CHADEMA kwa umma wa watanzania ikiwemo kuzusha kuwa upo uwezekano wa CHADEMA kupewa fedha hizo kwa mikataba yenye masharti ya kuiweka nchi rehani.


Tayari ameshaandikiwa barua ya kisheria tarehe 24 Agosti 2012 ya kumtaka aombe radhi na kulipa fidia ya bilioni tatu kwa matamshi hayo ya uzushi na uongo yenye maana ya kuwapotosha waliyoyasikia na kuyasoma kuwa CHADEMA kinawalaghai wananchi, kina viongozi wasio waaminifu na kwamba kiko tayari kuuza nchi wa uroho wa madaraka.


Kipaumbele cha CHADEMA katika suala hili ni kuombwa radhi hata hivyo kiwango cha fidia ya fedha kwa fedheha kilichotakiwa ni fundisho kuwa uzushi na uongo unagharimu.


Ikumbukwe kwamba tarehe 12 Agosti 2012 nilitoa kauli ya awali baada ya mkutano Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM na waandishi wa habari ambapo pamoja na mambo mengine nilieleza kwamba tutatoa tamko la kueleza hatua za ziada baada ya kupata taarifa kamili aliyoitoa.


Katika kauli hiyo nilitoa mwito kwa Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete kueleza watanzania iwapo propaganda hizo chafu zina baraka zake; hivyo ukimya wake mpaka sasa kuhusu matamshi hayo inakifanya CHADEMA kuwa na imani yenye shaka (benefit of doubt) kwamba Nape hakutumwa na chama chake kutoa matamshi aliyoyatoa.


CHADEMA inachukua fursa hii kuutaarifu umma kwamba asipotekeleza matakwa hayo ndani ya siku saba kuanzia tarehe hiyo aliyopokea barua hatua nyingine ya kumfikisha mahakama kuu zitaanzishwa ili aweze kuchukuliwa hatua zaidi.


Pamoja na kuchukua hatua za kisheria, CHADEMA kinaendelea kutimiza dhima yake ya kuleta uongozi bora, sera sahihi, mikakati makini na oganizesheni thabiti kwa maendeleo endelevu ya Tanzania kwa pamoja na mikakati mingine kutekeleza operesheni ya vuguvugu la mabadiliko nchini (M4C) na tunawashukuru wananchi kwa kuendelea kuunganisha nguvu ya umma kwa hali na mali katika maeneo mbalimbali nchini.


Imetolewa Tarehe 26 Agosti 2012 na:


John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi

TASWIRA HALISI YA UZINDUZI WA TAMASHA LA FIESTA MJINI MOSHI

Wasanii machachari Bongo Move Wema Sepetu (kushoto) na Aunt Ezekiel wakicheza muziki wa bongo Fleva uliokuwa ukishushwa na Msanii wa Bongofleva,Ferooz katika uzinduzi wa Tamasha la Serengeti Fiesta 2012 Bhaaaaass! katika Uwanja wa Chuo cha Ushirika Mjini Moshi usiku huu. Tamasha hilo limebamba ile mbaya.
Ferooz akiwa na mmoja wa mashabiki wake wakilishambulia jukwaa vilivyo.
Sehemu ya wakazi wa mji wa Moshi wakiendelea kushuhudia makamuzi ya wasanii mbalimbali wanaotumbuiza usiku huu kwenye uzinduzi wa tamasha la Serengeti Fiesta 2012.
Prezoo akiwarusha mashabiki kibao (hawapo pichani) waliojitokeza jioni ya leo kwenye uzinduzi wa tamasha la Serengeti Fiesta 2012
Pichani juu na chini ni mwanamuziki kutoka nchini Kenya na mmoja wa shiriki wa shindano la Big Brother Stargame,CMB Prezoo akitumbuiza jukwaani usiku huu kwenye uzinduzi wa tamasha la Serengeti Fiesta 2012 ndani ya uwanja wa chuo cha ushirika mjini Moshi.
Mmoja wa wasanii wa hip hop Joh Makini akikamua vilivyo usiku huu mbele ya umati mkubwa wa watu uliojitokeza kwenye uzinduzi wa tamasha la Fiesta.
Msanii mahiri wa bongofleva,Lina akiwa na densaz wake wakilishambulia jukwaa vilivyo.
Lina akiimba wimbo wake Yalaiti
Mkali mwingine wa hip hop Mwana FA akishusha mitindo huru.
Pichani juu na chini Mwana FA akilishambulia jukwaa vilivyo kwa mitindo yake huru iliyokuna vilivyo mashabiki wake,waliofika kwa wingi kwenye tamasha la Serengeti Fiesta 2012.
Wasanii wa nyota wa Filamu hapa nchini nao walijumuika kwa pamoja kwenye uzinduzi wa tamasha la Serengeti Fiesta 2012,pichani jukwaani ni Wema Sepetu,Jacob Steven a.k.a JB,pamoja na Aunt Ezekiel wakilisakata sebene.
Ray nae akilisakata sebene vilivyo.

CHADEMA WAWASHA MOTO IGUNGA


Katibu Mkuu wa Chamacha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa akiwahutubia wananchi wa mji wa Igunga na vitongoji vyake, katika mkutano wa hadhara wa kuwashukuru wananchi kwa ushiriki wao katika kufanikisha kesi ya uchaguzi wa jimbo hilo, uliofanyika kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini Igunga jana.
YAFANYA MKUTANO MKUBWA IGUNGA KUSHUKURU WAPIGAKURA,DK SLAA AIONYA CCM IKIKATA RUFAA ITAUMBUKA
Mustapha Kapalata, Igunga
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jana kilitikisa Jimbo la Igunga mkoani Tabora, kwa kufanya mkutano mkubwa wa hadhara ikiwa ni mara ya kwanza tangu Mahakama Kuu Kanda Tabora kutengua ubunge wa Dk Dalaly Kafumu wa Chama Cha Mapinduzi, huku kikiionya CCM kuwa kitaumbuka iwapo kitakata rufaa kwa uamuzi huo wa mahakama.

Akizungumza katika mkutano huo uliofanyika katika Viwanja vya Sokoine, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa alisema CCM kisithubutu kukata rufaa kwani kitaumbuka kwa kuwa kilicheza faulo nyingi katika uchaguzi huo.

Alisema ameshangazwa na kauli ya CCM kusema kuwa kitakata rufaa katika kesi hiyo wakati kisheria, kwa kesi za uchaguzi na pia katika hatua hiyo chama hakina nafasi yoyote bali mgombea au mwanachama wa chama husika, ndiye anayeweza kwenda mahakamani kufungua kesi na kupinga.

Katika mkutano huo uliofurika maelfu ya wanachama na washabiki wa wa chama hicho, Dk Slaa alisema kuwa Chadema kitakiangusha vibaya CCM hata ikiwa uchaguzi katika Jimbo la Igunga utarudiwa.

Huku akitoa mifano mbalimbali ya jinsi baadhi ya wanachama wa CCM walivyokuwa wakitoa rushwa, Dk Slaa alimtuhumu Mweka Hazina wa chama hicho, Mwigulu Nchemba, ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi kwamba alikuwa kinara wa kutoa rushwa katika kampeni za uchaguzi mdogo wa Igunga Oktoba mwaka uliopita.

“Chadema imejipanga kwa rufaa hiyo ya CCM ikiwa ni pamoja na kufungua kesi nyingine dhidi ya vigogo wa CCM, walioshiriki katika kampeni za uchaguzi huo,”alisema Dk Slaa.

Dk Slaa pia alimponda Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama akieleza kuwa mdomo wake umemponza kwa sababu alikuwa akizungumza mambo ambayo hakujua madhara yake.

Wakati akitoa hukumu ya kesi hiyo, Jaji Mary Nsimbo Shangali wa Mahakama Kuu alisema moja ya hoja saba zilizotolewa na Chadema ambayo mahakama iliikubali ni ile ya Mukama kudai Chadema kilipeleka makomandoo katika uchaguzi huo na kupanga kuuvuruga.

Dk Slaa alisema: “Mukama alikurupuka kwa kutamka maneno bila kufanya utafiti hali iliyosababisha CCM kupoteza jimbo.”

Alikwenda mbali zaidi na kueleza kuwa suala la CCM kuingiza silaha ndani ya nchi, bila kibali wala leseni na kuwapatia vijana wake mafunzo katika kambi za Ilemo, Iramba mkoani Singida linamhusu mwenyekiti wa chama hicho na siyo mtu mwingine.

Alidai kuwa wakati wa uchaguzi wa Igunga, vijana hao walikuwa wakipewa mafunzo ya kijeshi akisisitiza kuwa suala hilo linamhusu mwenyekiti wa chama hicho akimtaka atoe majibu na ufafanuzi juu ya hilo.

Dk Slaa alisema kuwa siku ya jana ilikuwa ni kwa ajili ya wananchi wa Igunga kusherehekea na kupongezana kwa mshikamano waliouonyesha wakati wote wa kusikilizwa kwa kesi hiyo, huku akitoa pongezi kwa mawakili waliosimamia kesi hiyo kwa kuiwakilisha vyema Chadema katika kesi hiyo.

Naye upande wake aliyekuwa mgombea wa Chadema katika uchaguzi mdogo wa Igunga Oktoba mwaka uliopita, Joseph Kashindye aliwashukuru wananchi walioiunga mkono Chadema akieleza kuwa wameonyesha ushirikiano mkubwa uliokipa ushindi chama hicho kikuu cha upinzani nchini.

Kashindye aliwashukuru pia wananchi wa Igunga kwa kukichangia Chadema Sh6 milioni zilizosaidia kulipia gharama za kesi hiyo pamoja na malazi kwa mashahidi mbalimbali waliotoa ushahidi kwenye kesi dhidi ya CCM iliyotolewa hukumu wiki iliyopita kwa kutengua ushindi wa Dk Dalaly Kafumu wa CCM.

“Mahakama imetenda haki kwa kuwa imetoa hukumu ya haki…, nimeamini kuwa haki ya mtu haipotei. Awali nilidhani kuwa mahakama ni mali ya CCM kumbe si kweli,” alisema Kashindye na kushangiliwa na mamia ya watu waliofurika katika uwanja huo.

Kashindye aliponda ahadi zilizokuwa zikitolewa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, Rais Mstaafu Benjamin Mkapa kwamba ndizo zilizofanya CCM kushindwa kesi.

“Watu wa ajabu sana, wametoa ahadi za kujenga madaraja, kusaidia chakula wakati hilo ni jukumu la Serikali,” alisema Kashindye akionyesha kushangaa.

Alibainisha kuwa wakati kesi hiyo ikinguruma mahakamani, alikuwa akitafutwa na wanachama wa CCM, lakini kutokana na kujua mbinu zao, aliamua kujichimbia kusikojulikana.

Dk Kafumu aliibuka mshindi katika uchaguzi huo mdogo uliofanyika Oktoba 2, mwaka jana kuziba nafasi ya Rostam Aziz ambaye alijiuzulu kwa madai kwamba anaachana na siasa chafu ndani ya CCM.

Katika uchaguzi huo kulikuwa na upinzani mkubwa kati ya Dk Kafumu na aliyekuwa mgombea wa Chadema, Joseph Kashindye ambaye hakuridhishwa na mwenendo wa uchaguzi huo, hivyo kuamua kupinga matokeo hayo mahakamani. Kesi hiyo ilifunguliwa Machi 26, mwaka huu
Chanzo:mwananchi.co.tz

Saturday 25 August 2012

CCM WAMNYOOSHEA KIDOLE MKAPA: NI KUTOKANA NA UTATA ULIOTOKANA NA MAHAKAMA KUTENGUA UBUNGE WA DK. KAFUMU


Fidelis Butahe na Leon Bahati
KITENDO cha Mahakama Kuu Kanda ya Tabora kutengua matokeo ya ubunge Jimbo la Igunga yaliyompa ushindi Dk Dalaly Peter Kafumu (CCM), kimeibua mvutano mwingine ndani ya CCM, ambapo sasa baadhi ya makada wake wameanza kumnyooshea kidole Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na baadhi ya mawaziri kuwa ndiyo chanzo cha kushindwa huko.
Baadhi ya makada maarufu na wenye uzoefu wa muda mrefu ndani ya chama hicho tawala, kwa nyakati tofauti kwenye mahojiano na Mwananchi Jumapili wamekiri kwamba, imefika mahali ambapo CCM inapaswa ijitazame na kuwa makini juu ya watu inaopaswa kuwatumia katika kampeni zake.
Katika tathmini yao, makada hao wamemtaja Rais Mstaafu Mkapa na mawaziri kadhaa, wakisema kuwa CCM haikuwa makini katika kuwateua wasimame kwenye majukwaa kupiga kampeni za kisiasa. Walitaja moja ya sababu kuwa ni Mkapa na baadhi ya mawaziri hao mashuhuri kuwa siyo wanasiasa wa jukwaani bali ni watendaji.
Licha ya CCM kujaribu kumtumia rais huyo mstaafu na mawaziri hao kutokana na heshima iliyojengeka kwao mbele ya Watanzania walio wengi, tathmini ya makada hao inaeleza kuwa hoja zao katika kampeni ama ziliwapa mwanya wapinzani, hasa Chadema kuiumbua CCM kwenye propaganda za majukwaani, hata kisheria.
Walikuwa wakizungumzia chaguzi ndogo zilizofanyika hivi karibuni katika Jimbo la Arumeru na ule wa Igunga Oktoba mwaka jana, ambao licha ya CCM kushinda, wiki hii mahakama kuu ilitengua ushindi huo. Kuanguka Igunga Dk Kafumu aliibuka mshindi kwenye uchaguzi mdogo uliofanyika Oktoba 2, mwaka jana kuziba nafasi ya Rostam Aziz aliyejiuzulu kwa madai ya kuchoshwa na kile alichoita siasa za majitaka ndani ya CCM, lakini mahakama imetengua ushindi wake.
Uchaguzi huo ulikuwa wa ushindani mkubwa kati ya Dk Kafumu na aliyekuwa mgombea wa Chadema, Joseph Kashindye ambaye aliamua kupinga ushindi wa Dk Kafumu mahakamani akidai hakuridhishwa na mwenendo wa uchaguzi huo. Kashindye alifungua kesi hiyo Machi 26, mwaka huu. Wakati wa kampeni za uchaguzi huo vigogo mbalimbali wa CCM akiwamo Mkapa walipiga kambi Igunga na kushiriki mikutano mbalimbali ya kampeni, ambapo pamoja na mambo mengine walitoa kauli tata zilizosababisha CCM kushindwa katika kesi hiyo.
Mbali na Mkapa viongozi wengine waliotoa kauli hizo na sasa wananyooshewa vidole ni Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama na Mbunge wa Tabora, Ismail Aden Rage. Kauli tata ya Mkapa Wakili wa mlalamikaji, Profesa Abdallah Safari, Agosti 20 mwaka huu aliwasilisha mahakamani hapo zaidi ya malalamiko 13 dhidi ya Dk Kafumu na wenzake.
Mbali na kueleza yaliyozungumzwa na Dk Magufuli, Profesa Safari alidai hoja nyingine ni Baraza la Waislamu (Bakwata) Wilaya ya Igunga kuwakataza waumini wasiipigie kura Chadema na kwamba naye Rais Mstaafu Benjamin Mkapa alitoa ahadi ya kugawa mahindi kwa wananchi wa Igunga siku moja kabla ya uchaguzi ili waichague CCM. Makada waonya

Mbunge wa Kahama, James Lembeli alisema kuwa utaratibu wa sasa wa chama hicho kuwatumia viongozi wastaafu umepitwa na wakati kwa sababu Watanzania wa sasa hawahitaji kusikia maneno mengi, bali sera. Alisema kuwa CCM inatakiwa itazame ilipojikwaa na kuacha kutafuta mchawi kwa kuwa matatizo yaliyokifikisha chama hicho kilipo sasa yanajulikana.
“Kampeni za CCM hivi sasa hazina maandalizi, kila anayeweza kuzungumza anachukuliwa na kujumuishwa kwenye kampeni, jambo ambalo siyo sahihi,” alisema Lembeli na kuongeza: “Inatumia watu bila kuangalia kama wanakubalika, katika chaguzi zinazokuja, chama kiwatumie makada wanaopendwa na wananchi na wenye uwezo wa kuuza sera za chama.”
Alitaja sababu nyingine ya CCM kuanguka hasa Igunga kuwa ni pamoja na mgawanyiko uliokuwapo ndani ya chama hicho baada ya baadhi ya makada kuzuiwa kushiriki katika kampeni hizo wakati wana mvuto kwa wapiga kura. Akitolea mfano watu hao alisema kuwa ni pamoja na Mbunge wa Urambo Mashariki, Samuel Sitta, ambapo alibainisha kuwa waliotoswa katika kampeni hizo wasingeweza kuishiwa maneno ya kuzungumza na kuanza kutoa ahadi zinazovunja sheria ya uchaguzi.
Dk Kigwangallah Akizungumzia suala hilo, Mbunge wa Jimbo la Nzega, Dk Hamisi Kigwangallah alisema kitendo cha CCM kutumia vigogo akiwamo Rais mstaafu Mkapa katika uchaguzi wa Igunga, ndiyo chanzo cha kushindwa kwa kesi hiyo kwa kuwa walizungumza mambo yasiyo na msingi wowote. Dk Kigwangallah ambaye Agosti 22 alichukua fomu za kuwania kiti cha Uenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa alisema kuwa uchaguzi mwingine ukifanyika katika jimbo hilo, viongozi na wabunge kutoka mikoa ya Tabora, Mwanza na Shinyanga ndiyo waachwe kufanya kampeni.
“Ni kweli CCM tuliweka watu wengi, ambao walipunguza kura za chama, lakini pia walizungumza mambo yasiyostahili,” alisema Dk Kigwangallah na kuongeza: “Uchaguzi ujao Igunga wasituletee watu kutoka CCM taifa, wanakuja na helikopta na kutumia gharama kubwa halafu mambo yanaharabika. Nadhani tubadilishe hali hii.”
Hata hivyo, alisema kuwa CCM inakubalika kwa kiasi kikubwa mkoani Tabora, hasa katika Jimbo la Igunga na kwamba kama Dk Kafumu akigombea tena, ataibuka mshindi kwani anakubalika na alishafanya mambo ya maendeleo.
Ibrahim Kaduma Kada mkongwe wa chama hicho, Ibrahim Kaduma alipoulizwa iwapo moja ya sababu za CCM kushindwa ni kuwatumia vigogo ambao siyo mahiri katika siasa za jukwaani, hakuwa tayari kulizungumzia suala hilo akitaka aachwe. “Naomba uniache kwanza, masuala haya yanatosha …, naomba uniache tafadhali kwa hisani yako tu,” alisema Kaduma. Ole Moloimet Naye Lepilal Ole Moloimet, kada wa CCM aliyewahi kushika nafasi mbalimbali ndani ya CCM na Serikali, alikilaumu chama chake kwa tabia ya kumtumia Rais Mstaafu Mkapa na baadhi ya mawaziri kwenye kampeni za uchaguzi.
Alisema kitendo cha kuwatumia watu hao licha ya kusababisha wadhalilike kinaonyesha udhaifu wa watu wanaoiongoza CCM hivi sasa. "Suala la kuwatumia marais wastaafu, kuwatumia mawaziri ni udhaifu wa viongozi wa CCM wanaoiongoza hivi sasa," alisema Moloimet. Akizungumzia uchaguzi wa Arumeru alisema: “Mkapa alidhalilishwa na mgogoro wa ardhi wa muda mrefu. …Wananchi walihoji kama alishindwa mgogoro huo wakati wa utawala wake, akizungumzia suala hilo sasa atakuwa anawaongopea."
Alisema kimsingi marais wastaafu hawapaswi kutumiwa kwenye siasa, badala yake iwe ni matukio muhimu yanayohusu Watanzania wote au juu ya uhusiano wa kimataifa kama vile mgogoro wa mpaka na Malawi. "Imefika mahali hawa viongozi wastaafu hata wakiombwa wakanadi sera majukwaani wao wenyewe wanapaswa wajipime. Si kila kitu wakubali," alisema Moloimet.
Tuvute subira- Mgeja Hata hivyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Hamisi Mgeja alisema: “Nadhani tuvute subira kwa sababu tukianza kunyoosheana vidole nani hakufaa nani alifaa itakuwa siyo jambo zuri, kama ni hivyo mbona tulivyoshinda Igunga hawakuwalaumu walioshiriki katika kampeni.”
Lusinde: Hakuna tatizo
Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde alisema kuwatumia wazee katika chaguzi za chama hicho hakuna tatizo, akiamini kuwa Jimbo la Igunga ni mali ya CCM na kwamba uamuzi wa kukata rufaa au kutokata anamwachia Dk Kafumu. “Natamani kama uchaguzi ungefanyika tena ili twende tukalichukue jimbo,” alisema Lusinde.
Sababu za kutenguliwa matokeo Akitoa hukumu hiyo, Jaji Mary Nsimbo Shangali alisema Mahakama ilipokea malalamiko 15 ambayo yaliridhiwa na pande zote mbili lakini baadaye yakaongezwa madai mengine mawili hivyo kufikia 17. Alisema hoja zilizothibitishwa na Mahakama ambazo zilizotumika kutengua matokeo hayo ni saba kati ya 17.
Baadhi ya hoja hizo ni pamoja madai kwamba Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli alitumia nafasi yake ya uwaziri kutoa ahadi ya ujenzi wa Daraja la Mbutu, ambalo lilikuwa ni moja ya kero kubwa kwa wananchi wa Jimbo la Igunga. Jaji Shangali aliikubali hoja nyingine ya washtaki kuwa ni ugawaji wa mahindi ya kuwawezesha wakazi wa Igunga kukabiliana na njaa wakati wa uchaguzi huo kwamba ulitumiwa vibaya na baadhi ya wanasiasa kuwashawishi wananchi wawapigie kura.
Mbali na Dk Kafumu, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya uchaguzi walikuwa ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Igunga aliyetangaza matokeo hayo.
Kauli ya Nape Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kwamba haoni kuwa kauli za Rais Mkapa, Magufuli, Mukama ndizo zilizokiangusha chama hicho alisema: “Ndiyo maana tunataka kukata rufaa kwa sababu hatukubaliani na hiyo hoja.”
Vita ya kuwania uongozi
Katika hatua nyingine, upepo wa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya CCM umezidi kushika kasi baada ya Mbunge wa Jimbo la Kahama, James Lembeli kuchukua fomu ya kugombea Uenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga huku akitamba kuwa ameingia kwa lengo la kumaliza makundi ya kisiasa yaliyokithiri ndani ya chama hicho.
Lembeli amechukua fomu sambamba na mpinzani wake mkubwa kisiasa Khamis Mgeja, ambaye kwa sasa ndiye mwenyekiti wa CCM mkoani humo. Mbali na vigogo hao, mbunge wa zamani wa Shinyanga mjini Leonard Derefa naye alichukua fomu za kuwania nafasi hiyo.
Wengine ni Teresia Kashinje, Bonaventure Mguziki, Regina Masanja na Alex Seseja. Hata hivyo, katika kinyang’anyiro hicho wagombea wanaoonyesha kuvutia hisia za wanaCCM wa Shinyanga ni Lembeli na Mgeja, ambao wamekuwa mahasimu wa siku nyingi katika siasa za mkoa huo, huku wote wakitoka wilayani Kahama.
Katika majigambo yao Lembeli amekuwa akinukuliwa na vyombo vya habari akitamba kuwa atahakikisha anamng’oa Mgeja katika nafasi hiyo huku Mgeja naye akidai hasimu wake huyo ni ‘sisimizi’ ambaye hamnyimi usingizi.
Makada wengine wa chama hicho waliochukua fomu za kuwania nafasi mbalimbali ni pamoja na Mkurugenzi wa Uchaguzi CCM Makao Makuu, Matson Chizii ambaye amejitosa kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Chama Mkoa wa Dar es Salaam. Wengine waliochukua fomu za kuwania nafasi hiyo mkoani Dar es Salaam ni John Guninita anayetetea nafasi hiyo na Mjumbe wa Nec, Ramadhan Madabida.

Naye Katibu wa Nec, Uchumi na Fedha na Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba amejitosa kuwania nafasi ya mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (Nec) kupitia kundi la viti 10 wakati Mbunge wa Mchinga, Said Mtanda akijitosa kuwania nafasi ya NEC kupitia Wilaya ya Lindi Vijijini. Aliyekuwa mbunge wa Misungwi, Dalali Shibiriti naye amechukua fomu ya kuwania Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) kupitia wilaya hiyo.
Uchaguzi huo pia umemwibua aliyekuwa Mbunge wa Busega, Dk Raphael Chegeni ambapo baadhi ya vijana wa wilaya hiyo walimchukulia fomu kuwania Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kupitia Wilaya ya Busega. Mbunge wa Jimbo la Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi naye amejitosa kuwania nafasi ya uenyekiti wa mkoa wa chama hicho mkoani Mbeya
Chanzo:Mwananchi.co.tz

NENO LA LEO NA MAGGID MJENGWA: TUNAPOSUBIRI KUHESABIWA NA DHANA YA KIUMBE NZITO


Ndugu zangu,
Kwa siku kadhaa nimekuwa nje ya mitandao. Hata magazeti, redio na televisheni zimenipitia kando. Jioni hii wakati nikipitia taarifa mbalimbali nimekutana na hili la hoja ya baadhi ya Waislamu kutaka sensa ya watu na makazi itakayofanyika kesho Jumapili igomewe kwa vile haina kipengele ama dodoso linalotaka kujua dini ya mtu.
Kabla sijatoa maoni yangu juu ya hilo ningependa niitafsiri dhana ya ‘ Kiumbe mzito’ kama tulivyoambiwa na wahenga wetu. Huenda si wengi kati yenu wasomaji wenye kufahamu maana hasa ya usemi wa Wahenga kuwa ‘ Kiumbe mzito’.
Ndio, Mwenyezi Mungu ametuumba wanadamu kwa usawa kwenye mambo mengi. Wala hakutaka kubagua; ona unyayo wa mwanadamu. U sawa, iwe kwa tajiri au masikini. Wewe na miye tumepata, ama wenyewe au kusikia mtu akilalamika kuwa soli ya kiatu chake imechakaa, kwamba anakwenda kwa fundi viatu kubadilisha soli. Lakini, wewe au miye hatujapata kumsikia mwanadamu mwenzetu akilalamika kuwa unyayo wake umechakaa, anataka kwenda kwa fundi awekewe unyayo mwingine!
Ndio, wewe na miye ama tumeshuhudia au kusikia kuwa upepo umeangusha mti, nyumba, ghorofa, gari na hata meli. Lakini, jiulize, je, umepata kumwona mwanadamu mwenzako anayetembea kwa miguu akiangushwa kwa upepo?
Binafsi hilo la mwanadamu kuangushwa na upepo sijapata kulisikia au kuliona kwa macho yangu. Mwanadamu hata awe mwembamba kiasi gani, haiyumkini akaangushwa kwa upepo. Na ukimwona mwanadamu mwenzako anaanguka barabarani, basi, ama ni mgonjwa, au ni mlevi. Na hilo la mwisho haliwezi kuwa na maana ya mwanadamu huyo kaangushwa na upepo, bali kaangushwa na pombe alizokunywa.
Naam, kiumbe mzito.
Na kesho ndio siku yenyewe ya Watanzania kuhesabiwa. Kuna wenzetu hususan kwenye Uislamu wenye kudai kuwa watagoma kuhesabiwa; Kisa? Hakuna dodoso lenye kutaka kujua dini ya mtu. Mimi naamini walioamua suala la dini ya Mtanzania lisiingizwe kwenye sensa walifanya uamuzi wa busara na wenye hekima sana.
Sisi ni Watanzania. Ni watu wamoja kwa asili. Na tujiulize kwanza; kwa nini tunahitaji kujihesabu. Ndio, sensa ina maana ya kujua idadi yetu kama Watanzania ili iisaidie Serikali katika kupanga mipango ya maendeleo ya nchi yetu. Mipango ya maendeleo ya nchi haibagui dini ya Mwananchi. Kama ni huduma ya maji, basi, maji hayo watakunywa Watanzania; wawe Waislamu, Wakristo, Wahindu au Wapagani. Hivyo hivyo kwa huduma nyingine muhimu za kijamii.
Bila shaka, Sensa ya watu na makazi ni mpango madhubuti wa Serikali kwa maendeleo ya watu wake na wenye kugharimu mabilioni ya shilingi. Si busara na hekima kwa baadhi ya viongozi wa madhehebu ya dini kushiriki kuhujumu mpango huu wa Serikali kwa manufaa ya wananchi wakiwamo waumini wa dini mbali mbali na hata wasio waumini. Na kubwa zaidi hapa ni ukweli huu; kuwa nchi yetu haina dini.
Naam, kiumbe mzito, hata kama Sensa ingeingiza kipengele cha dini, basi, wangetokea wachache wa kuhoji; iweje leo watu wakaulizwa dini zao, ama ni njama za kutaka kuwabagua na kuwakandamiza zaidi kimaendeleo Watanzania wa dini fulani au ni mbinu ya kutaka kudhibiti kuongezeka kwa idadi ya waumini wa dini fulani. Ndio, kuna ambao wangepambana kutaka kipengele cha dini kiondolewe na hata kutishia kugomea sensa.
Naam, kiumbe mzito, na mgumu pia!
Shime Watanzania na hususan ndugu zangu Waislamu, kesho ikifika na tuwe tayari kuhesabiwa kwa maendeleo ya nchi yetu. Kwa maendeleo yetu.
Mungu Ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania.
www.mjengwablog.com

AL-SHAABAB YAAMUA KUUZA NYAMA YA FISI ILI KUGHARIMIA OPERESHENI ZAO ZAKIJESHI

 
Wafanya biashara wa al-Shabaab wanawaambia wakaazi wa Kismayu kuwa kula nyama ya fisi itawalinda na maradhi na jicho la uovu. Juu, mwanamke anauza nyama huko Dinsor. [Na Simon Maina/AFP]
Wafanya biashara wa al-Shabaab wanawaambia wakazi wa Kismayu kuwa kula nyama ya fisi itawalinda na maradhi na jicho la uovu. Juu, mwanamke anauza nyama huko Dinsor. [Na Simon Maina/AFP

Na Adnan Hussein, Mogadishu

Al-Shabaab wameanza kuuza nyama ya fisi katika mji wa bandari kusini ya Somalia kama njia ya kukusanya pesa kwa ajili ya operesheni za kijeshi kabla ya kukaribia kwa vita dhidi majeshi ya Somalia na washirika wake , wachambuzi wasema.

Masheikh wa Somalia ambao kwa karne nyingi wamekuwa wakichukulia kuwa ulaji wa nyama ya fisi kulikatazwa na Uislamu kwa vile mnyama huyu hula miili ya maiti wa kibinadamu na wanyama.
Hatua hii mpya ni moja ya dalili nyingi za kuchanganyikiwa kifedha kwa washirika wa kikundi cha al-Qaida wakati majeshi ya Somalia na washirika wake yanaendelea kuziteka kambi za al-Shabaab nchini kote.
Ili kuwashawishi wakaazi kula nyama hiyo, ambayo mara nyingi ina magonywa kwa sababu mnyama huyo anakula mizoga, wafanya biashara wa al-Shabaab wamekuwa wakitumia uchawi wa asili ili kuwanasa wale wasiofahamu vyema, alisema Suleiman Abdi Guled, mpishi katika Hotel Alkhalej mjini Mogadishu ambaye ana familia huko Kismayo.
Kwa mujibu wa watu wanaofanya uchawi, nyama ya fisi ni nzuri kwa kujikinga na maapizo na dhidi ya magonjwa na jicho la ubaya.
"Ni ishara ya kutisha kwa sababu ni nje ya mila [za Kisomali] kula nyama ya fisi, hasa kwa vile wapo wanyama wengine wa kuliwa," alisema. "Al-Shabaab ni kikundi kilichopotea ambacho kinajaribu kutumia fisi na uchawi kwa operesheni zao za kijeshi."
Khalif Mohamud, mfanya biashara wa Kismayo, alisema al-Shabaab wanapata pesa katika biashara hii kwa kuudhibiti uchinjaji wa fisi.
"Al-Shabaab wanayo majumba ya machinjio mjini na tunalazimika kulipa pesa kwa kuchinja na kuchuna wanyama baada ya mawindo," aliiambia Sabahi.

Nyama ya fisi -- imeruhusiwa au kukatazwa kidini ?

Sheikh wa Somalia Sheikh Mohamud Awabdulle Ariif alisema watu wamekatazwa kuwinda na kula nyama ya fisi kwa mujibu wa sharia.
"Fisi ni miongoni mwa wanyama wadanganyifu na walafi, kwa vile wanawinda kondoo na kula nyama ya binadamu," alisema. "Pia hufukua makaburi na kutoa na kula maiti, pamoja na kula mizoga ya wanyama, wadudu na mabaki ya mawindo mengine."
Mursal Issac, mwanaharakati wa jumuiya ya kiraia mjini Mogadishu, alisema hali mbaya ya kifedha ya al-Shabaab imekipelekea kikundi kuamua kufanya biashara ya mkaa na nyama ya fisi ili kugharimia operesheni zake za kijeshi.
"Fisi ni wanyama wachafu wanaokula mizoga ya wafu, na ndio sababu ninawataka ndugu zetu wa Kismayo kujizuia na kula nyama yao," aliiambia Sabahi. "Tumebarikiwa na Mungu ardhi na wanyama wa baharini, na nadhani ni bora kujiweka mbali na mnyama huyu."
Issac alisema al-Shabaab inajaribu kunyanyua hali yake mbaya ya kifedha kwa sababu inaogopa kushindwa kijeshi mikononi mwa Jeshi la Somalia na Misheni ya Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM).
Sagal Hassan Ali, ambaye anafanya kazi katika mkahawa mdogo katika kiunga cha Via Afmadow, Kismayo, alisema yeye hatakula nyama ya fisi na hata asingewinda mnyama huyu muovu.
Aliiambia sabahi kuwa anachukizwa kuwa soko la hapo limegeuzwa uwanja wa kufanyia biashara ya nyama hii.

Al-Shabaab kinavunjikavunjika

Mtaalamu wa kijamii Mana Moalim Ino alisema kuuza nyama ya fisi katika masoko ya Kismayo ni kwa ajili ya maslahi ya wanamgambo ambao wamechukua silaha dhidi ya serikali ya Somalia na majeshi ya AMISOM.
Hata hivyo, aliiambia Sabahi kuwa kushindwa na kuchanganyikiwa kunakoukabili uongozi wa al-Shabaab kutaleta ushindi kwa vikosi vishiriki.
Ino alisema kuwa jeshi la Somalia, likisaidiwa na AMISOM, litawatimua al-Qaida na wafuasi wao wa Kisomali kutoka maficho yao huko Kismayo, Marka , Boali, Baardheere na Jowhar.
"Mpaka sasa, majeshi yetu yamethibitisha ushiindi katika vita vyao dhidi ya al-Qaida," alisema. "Ushindi huu umetupa matumaini kuwa jeshi la Somalia bado linafanya vizuri, halikugagawanyika kwa misingi ya kikabila na halioneshi dalili ya kushindwa kipuuzi."
Katika miezi sita iliyopita, al-Shabaab imepoteza ngome zake muhimu mjini Mogadishu, pamoja na miji ya Afgoye , Balad na Afmadow . Vikosi vya washirika pia vimetoa vipigo vikubwa kwa Al-Shabaab huko maeneo ya Gedo, Juba ya Chini na Juba ya kati.
Kutokana na kushindwa kwao hivi karibuni, al-Shabaab imekuwa ikijihusisha na mbinu mpya, kuanzisha kampeni za propaganda na mashambulizi ya kigaidi nchini Kenya , na kuwaua waandishi wa habari mjini Mogadishu
Chanzo:Tis Day Magazine

Zitto:Kiama walioficha mabilioni Uswisi

Zitto Kabwe
ASEMA ATAFANYA HIVYO BUNGE LA OKTOBA KAMA SERIKALI ITASHINDWA, MABILIONI HAYO YAHUSISHWA NA UFISADI WA MEREMETA
Waandishi Wetu
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe ameahidi kuwataja wanaohusika kuficha mabilioni ya fedha nchini Uswisi katika kikao kijacho cha Bunge Oktoba, mwaka huu iwapo Serikali itashindwa kufanya hivyo hadi muda huo.
Wakati Zitto akisema hayo, kashfa hiyo imechukua sura mpya na sasa fedha hizo zinahusishwa na ufisadi katika Kampuni ya Meremeta.
Kauli ya Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, imekuja siku chache tangu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta kuwataka wanaowafahamu walioficha fedha hizo kuwataja hadharani ili iwe rahisi kwa Serikali kuwachukulia hatua.
Hata hivyo, Zitto akizungumza na gazeti hili jana alisema: “Mimi ni mbunge makini ninayefahamu taratibu za Bunge na kuheshimu haki za watu wengine, siwezi kukurupuka katika suala hili. Ninaiachia Serikali na vyombo vyake iendelee kulifanyia kazi na ikiwa watashindwa kuwataja wahusika, basi wasubiri kikao kijacho, nitaweka hadharani majina ya wahusika wote.”
Zitto alisisitiza kuwa Serikali ina uwezo wa kupata taarifa zozote inazozihitaji kutoka Uswisi na kwamba ndiyo maana ameipa muda wa kulifanyia kazi suala hilo kabla yeye hajachukua hatua ya kuwataja wahusika.
“Sikia, lazima tukubaliane jambo moja kwamba mimi siyo Serikali, wala sina dola, ndiyo maana nasema kwamba tusubiri utekelezaji wa ahadi ya Serikali, lakini wakishindwa kuwataja, basi mimi nitatumia nafasi yangu kama mbunge kuwataja na nitafanya hivyo ndani ya Bunge na wala siyo nje ya hapo,” alisema.
Uchunguzi zaidi wa gazeti hili umebaini kuwa kiasi cha Dola za Marekani 186 milioni (takriban Sh300 bilioni) kwa viwango vya sasa vya kubadilishia fedha ambavyo ni Sh1,600 kwa Dola ya Marekani, kimefichwa katika benki tatu tofauti za Uswisi.
Uchunguzi zaidi unabainisha kuwa takwimu hizo ni rasmi kwani zimetolewa na Benki Kuu ya Uswisi, lakini taarifa zaidi zinadai kuwa kuna fedha nyingi zaidi zilizofichwa na Watanzania katika benki nyingine nchini humo ambazo taarifa zake zinaweza kupatikana ikiwa Serikali itasimamia vizuri suala hilo.
Watanzania 27 wameripotiwa kumiliki fedha nchini humo, na mmoja wao anadaiwa kwamba anamiliki Dola za Marekani 56 milioni (wastani wa Sh89.6 bilioni).
Kashfa ya kuwapo kwa vigogo walioficha fedha zao Uswisi iliibuliwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini Juni mwaka huu na baadaye mwangwi wake kulitikisa Bunge katika Mkutano wake wa Nane uliomalizika hivi karibuni.
Habari hizo zilikuwa zikinukuu taarifa ya Benki Kuu ya Uswisi iliyoitoa na kuonyesha kuwapo kwa kiasi cha Sh315.5 bilioni zilizotoroshwa Tanzania na kufichwa nchini humo na vigogo ambao ni wanasiasa pamoja na wafanyabiashara.
Suala hilo pia lilijadiliwa katika kikao cha Bunge kilichopita, huku ikidaiwa kwamba fedha hizo zinatokana na biashara (deals) zilizofanywa na watendaji wa Serikali na wafanyabiashara kwenye sekta za nishati na madini na kwamba sehemu kubwa ya fedha zililipwa na kampuni za utafutaji mafuta na gesi katika Pwani ya Mkoa wa Mtwara zilizopewa mikataba kati ya mwaka 2004 na 2006.

Uhusiano na Meremeta

Habari zaidi zinadai kuwa fedha zilizofichwa Uswisi hivi sasa zina uhusiano na ufisadi kupitia Meremeta unaohusisha kiasi cha Dola za Marekani 132 milioni wastani wa Sh211.2 bilioni ambazo zilitoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kwenda Benki ya Ned Afrika Kusini.
Fedha hizo zililipwa kama marejesho ya mkopo wa Dola 10 milioni (sawa na Sh1.6 bilioni tu, uliokuwa umechukuliwa na Kampuni ya Meremeta Ltd ambayo ilikuwa mali ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), ikishughulikia uchimbaji wa madini.
Utata katika malipo hayo ni uhalali wa ongezeko la Dola 122 milioni katika malipo hayo, kwani mkopo wa Dola za Marekani 10 milioni ulirejeshwa na faida ya zaidi ya asilimia 1,000.

Uchunguzi unaonyesha kuwa fedha hizo za marejesho tata zilifichwa katika benki moja (jina tunalihifadhi) nchini Mauritius, na baadaye kati ya 2005 na 2006 zilihamishiwa nchini Uswisi, ambako sehemu yake zipo kwenye akaunti ya kigogo ambayo inaongoza kwa kuwa na kiasi kikubwa cha fedha, karibu Sh90 bilioni.
Kashfa ya Meremeta ni ya muda mrefu na mara nyingi Serikali imekuwa ikikataa kuizungumzia kwa maelezo kwamba ni suala ambalo lina masilahi ya usalama kwa taifa.
Awali, Serikali ilisema kwamba Meremeta Ltd ni kampuni ya Kitanzania iliyokuwa ikimilikiwa na JWTZ kwa ajili ya mradi wake wa Nyumbu, Mkoa wa Pwani.
Taarifa za usajili zilizotolewa na Msajili wa Kampuni wa Uingereza na Wales zinabainisha kuwa kampuni hiyo iliandikishwa nchini humo mwaka 1997 na baadaye ilifilisiwa hukohuko Uingereza mwaka 2006.
Taarifa ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela) ya Mei 31, 2005 inabainisha kwamba Meremeta Ltd ni tawi la kampuni ya kigeni iliyosajiliwa Tanzania, Oktoba 3, 1997 na kwamba hisa 50 za kampuni hiyo zilikuwa zinamilikiwa na Kampuni ya Triennex (Pty) Ltd. ya Afrika Kusini, wakati hisa 50 zilizobaki zilikuwa zinamilikiwa na Serikali ya Tanzania.
Utata kuhusu umiliki wa Meremeta Ltd unatokana na taarifa ya Brela ambayo pia inazitambua kampuni mbili za Kiingereza ambazo ni London Law Services Ltd na London Law Secretarial Ltd kuwa wamiliki wa hisa moja kila moja ndani ya Meremeta.
Licha ya Serikali kutokuwa mmiliki pekee wa kampuni hiyo, BoT ililipa madeni yote ya Meremeta badala ya kusaidiana na washirika wake ambao kisheria wanaonekana kuwa walikuwa wakimiliki hisa katika kampuni hiyo.
Serikali Tanzania ilikuwa ikimiliki asilimia 50 ya hisa na kwa mujibu wa taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), uhalali wa malipo hayo ulikuwa na walakini kwani kiutaratibu, Nedbank Ltd ilitakiwa iachwe idai fedha zake kutoka kwa mfilisi wa kampuni hiyo kama ilivyo kwa wadeni wengine.

Meremeta bungeni

Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini iliwahi kupewa idhini ya kuchunguza suala hilo, lakini Spika wa Bunge, Anne Makinda alilihamishia katika Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.
Hata hivyo, uchunguzi huo haukuwahi kufanyika na Ofisi ya Spika pia haijawahi kutoa taarifa yoyote. Hivyo suala hilo kubaki kitendawili hadi leo.
Hatua ya Spika kuridhia uchunguzi ilikuja baada ya mvutano wa muda mrefu, uliotokana na hoja zilizokuwa zikitolewa na Serikali kwamba suala la Meremeta lisingeweza kufanyiwa uchunguzi kutokana na “sababu za kiusalama.”
Kumbukumbu za Bunge zinaonyesha kuwa Zitto aliwahi kuwasilisha barua kwa Katibu wa Bunge akitoa taarifa ya hoja ya kutaka kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge kwa ajili ya kuchunguza tuhuma za ufisadi kupitia kampuni hiyo ya uchimbaji wa dhahabu.
Zitto alitoa taarifa ya mdomo bungeni Julai 13, mwaka jana kwa mujibu wa Kanuni ya Bunge Namba 117 (2)-(a) inayomruhusu kutoa taarifa ya kusudio lake la kuwasilisha hoja ya kutaka Bunge liunde kamati teule.
Aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi (sasa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii) aliwahi kusema bungeni kwamba halifahamu suala hilo kwenye majumuisho ya Bajeti ya wizara hiyo ya 2011/12
Chanzo:www.mwananchi.co.tz