Subscribe:

search

.

Sunday 26 August 2012

NAIL Armstrong BINADAMU WA KWANZA KUFIKA MWEZINI AFARIKI DUNIA



 Hussein Issa ,Mashirika
NAIL Armstrong linaweza lisiwe jina maarufu enzi hizi, lakini hilo ndilo jina lililoshika chati mwishoni mwa miaka ya 1960 kwani alikuwa binadamu wa kwanza kukanyaga mwezini.Hata hivyo gwiji huyo wa mambo ya anga , amefariki akiwa na umri wa miaka 82 akiacha rekodi yake hiyo iliyotikisa dunia.
Neil Armstrong alitua mwezini Julai  20, 1969 akiwa katika chombo kilichoitwa Apollo na kusema ''hiyo ilikuwa hatua ndogo ya binadamu, lakini mapinduzi makubwa kwa ubinadamu''.
Armstrong na mwanaanga mwenzake Buzz Aldrin walitumia saa mbili na nusu wakitembea juu ya mwezi .  Neil Armstrong na wanaanga wenzake watatu Novemba mwaka 2011, walitunukiwa tuzo ya Congressional Gold Medal ambayo ndiyo ya juu zaidi inayotolewa kwa raia nchini Marekani.  Armstrong amefariki  dunia jana katika hospitali ya Columbus jimboni Ohio ambako alifanyiwa upasuaji wa moyo mapema mwezi huu.
Kulingana na wasifu wa Armstrong ambao umechapishwa na Shirika la Anga la Marekani, NASA, mwanaanga huyo aliyezaliwa jimboni Ohio mwaka 1930, alisafiri kwa ndege kwa mara ya kwanza akiwa na miaka sita, na kupata leseni ya kuendesha ndege akiwa na miaka 16, hata kabla ya kujua kuendesha gari.  Alitumikia Jeshi la Marekani kama rubani wa ndege za kivita wakati wa vita vya Korea, na baadaye akajiunga na masomo ya sayansi ya anga.   Baadaye aliajiriwa kama rubani wa kuzifanyia ndege majaribio.

Neil Armstrong alijiunga na programu ya anga mwaka 1962, na kurusha chombo cha kwanza cha anga miaka minne baadaye.   Aliteuliwa kuwa kiongozi wa wanaanga walioshiriki katika safari ya Apollo, ambayo iliwafikisha wanadamu wa kwanza mwezini.

Hatua yake ya kwanza mwezini iliangaliwa na mamilioni ya watu duniani kwa njia ya televisheni.Baada ya kutangazwa kwa kifo cha mwanaanga huyo, Mkuu wa Shirika la Anga la Marekani, NASA, Charles Bolden ametuma salamu zake za rambirambi kwa familia ya Armstrong.Charles Bolden amesema wakati wowote kutakapokuwa na vitabu vya historia, jina la Neil Armstrong litaandikwa kwenye kurasa za vitabu hivyo.
Amesifia jinsi Neil Armstrong alivyoishi maisha ya unyenyekevu, na kusema kuwa mfano wake ni wa kuigwa.   Pia Rais Barack Obama  wa Marekani ametoa salamu za rambirambi zake, na kusema mwanaanga huyo ni miongoni mwa mashujaa wakubwa wa Marekani.Amesema Armstrong pamoja na wenzake 11 katika chombo cha Apollo, walibeba matarajio ya taifa zima la Marekani katika safari yao ya anga mwaka 1969.
''Waliionyesha dunia ari ya Marekani kuangalia mbali zaidi ya yale yanayofikirika, na kuthibitisha kuwa penye juhudi na maarifa, kila kitu kinawezekana,'' amesema Obama, na kuongeza kuwa ujumbe alioutoa Armstrong baada ya kukanyaga kwenye ardhi ya mwezini, ni mafanikio ya binadamu ambayo kamwe hayatasahaulika.
Katika tangazo lililotolewa na familia ya Armstrong kufuatia kifo chake, mwanasayansi huyo ametajwa kuwa shujaa wa Marekani, ambaye muda wote yeye alisisitiza kuwa alichokifanya kilikuwa wajibu wake kikazi.  Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Familia yake imesema kuwa kifo chake kimetokana na matatizo yaliyofuatia upasuaji wa moyo.
Familia ya Armstrong imesema kuwa mwanaanga huyo aliendelea kufuatilia maendeleo ya safari za anga, na kila alipofanya hivyo shauku yake ya ujana ilijitokeza tena.  Neil Armstrong alistaafu kutoka NASA mwaka 1971 na alifanya kazi kwenye bodi ya wakurugenzi.   Hakupenda kuwa mtu wa kujionyesha onyesha, isipokuwa mara chache tu kwenye kumbukumbu za safari ya kwanza mwezini, au akiunga mkono kuendelea kwa utafiti wa anga.

Familia yake imesema kuwa, ingawa Neil Armstrong alipenda kuishi maisha yake bila bugudha, alifurahia ujumbe wenye nia njema kutoka kila pembe ya dunia kuhusu yeye na wenzake

Chanzo:Mwananchi.co.tz

0 comments: