Subscribe:

search

.

Wednesday 15 August 2012

MWENYEKITI WA BALAZA LA VIJANA CHADEMA AHOJIWA NA POLISI


Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha),John Heche
Boniface Meena na Fredy Azzah
MWENYEKITI wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha), John Heche amehojiwa na polisi kwa saa nne kwa madai kuwa alitoa lugha za matusi dhidi ya Rais Jakaya Kikwete kwa kumwita ombaomba.Taarifa zilizolifika gazeti hili jana zinaeleza kuwa Heche alihojiwa na polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime-Rorya. Anadaiwa kutoa lugha hiyo ya matusi katika mkutano wa hadhara alioufanya Jumamosi iliyopita, Sirari mkoani Mara.

Ilielezwa kuwa baada ya mkutano huo uliofanyika kwenye Viwanja vya Sirari kumalizika, Heche alipigiwa simu na polisi akitakiwa kwenda kutoa maelezo kuhusu kauli yake hiyo dhidi ya Rais Kikwete.

Mwenyekiti huyo wa Bavicha aliliambia gazeti hili jana kuwa, "Nilihojiwa jana (juzi) kuanzia saa 11:00 jioni hadi saa 2:30 usiku na polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime Rorya."
Aliendelea kusema, “Aliyenihoji ni OC CID wa Wilaya ya Kipolisi Sirari ambaye anadai kuwa, kumwita Rais ombaomba ni lugha ya matusi.”

Heche alikiri kufanya mkutano huo eneo la Sokoni, Sirari mkoani Mara na akasema alishangaa kupigiwa simu na polisi akiitwa kwenda kutoa maelezo baada ya mkutano huo kumalizika.“Siku hiyo sikwenda kwa kuwa sikuwa na mwanasheria wangu kwa hiyo nikawaambia kuwa ningefika baada ya kuwa naye hivyo jana (juzi) nikaenda,” alisema Heche.

Alisema siku ya kwanza kufika polisi alikutana na viongozi wa ngazi ya juu wote wa Kanda Maalumu ya Tarime –Rorya, ambao walikuwa wakimsubiri kumhoji.

Kaimu Kamanda wa Polisi Tarime-Rorya, Sebastian Zacharia alithibitisha kuhojiwa kwa kiongozi huyo wa Chadema na kusema hii ni kutokana na taarifa kwamba alitoa maneno ya kashfa kwa kiongozi wa nchi.

“Alihojiwa juzi katika kituo cha Sirari na sasa tunakamilisha upelelezi,” alisema Kamanda Zacharia.
Kamanda huyo alisema hivi sasa wanakamilisha upelelezi wa suala hilo kabla ya kupeleka jalada kwenye ofisi ya mwanasheria wa serikali kwa ajili ya hatua zaidi.

“Siwezi kujua alihojiwa kwa kwa muda gani kwa sababu mahojiano yalifanyika huko Sirari, ila ninachoweza kusema tunamalizia upelelezi kabla ya kupeleka faili kwenye ofisi ya mwanasheria wa serikali kwa hatua zidi,” alisema Zacharia.

Kauli ya Kamanda huyo imekuja baada ya OC CID wa Wilaya ya Kipolisi Sirari, George Wilbard aliyemhoji Heche kusema kwamba, hawezi kuzungumzia suala hilo kwa kuwa yeye siyo msemaji wa polisi kwenye Kanda hiyo.
Chanzo:mwananchi

0 comments: