Subscribe:

search

.

Thursday 9 August 2012

RAIS KIKWETE AMTUMIA SALAM ZA RAMBIRAMBI MKUU WA MKOA WA TABORA KUFATIA AJALI YABASI LA SABENA LILILOUA WATU 17



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za Rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Fatma Abubakar Mwasa kufuatia taarifa za vifo vya watu 17 wakiwemo watoto watano vilivyosababishwa na ajali ya Basi la Kampuni ya Sabena iliyotokea katika eneo la Kitunda, Wilaya ya Sikonge Mkoani Tabora siku ya Jumanne tarehe 7 Agosti, 2012.
“Nimesikitishwa na kuhuzunishwa sana kutokana na taarifa za vifo vya watu 17 waliofariki papo hapo baada ya Basi la Abiria la Kampuni ya Sabena kupata ajali katika eneo la Kitunda Wilayani Sikonge katika Mkoa wa Tabora”, amesema Rais Kikwete katika Salamu zake za Rambirambi na kuongeza,
“Kwa mara nyingine tena tunashuhudia kupotea kwa maisha ya ndugu zetu 17 wasiokuwa na hatia kutokana na ajali za barabarani za mara kwa mara ambazo busara na hekima ya madereva na uwajibikaji wa pamoja wa vyombo vyenye dhamana na usimamizi wa Sheria ya Usalama Barabarani vinahitajika sana kuepusha vifo vya aina hii”.
“Kwa dhati ya moyo wangu, ninakutumia wewe Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mheshimiwa Fatma Mwasa Salamu zangu za Rambirambi na pole nyingi kutokana na msiba huo mkubwa uliotokea Mkoani kwako. Aidha naomba unifikishie rambirambi hizi kwa ndugu na jamaa wa watu wote waliofikwa na msiba huu. Nawaomba wote wawe na moyo wa uvumilivu na subira wakati huu wa kuomboleza vifo vya ndugu na jamaa zao. Ninawahakikishia kuwa niko pamoja nao katika maombolezo haya”, ameongeza kusema Rais Kikwete katika Salamu zake.
Amesema anamuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema azilaze mahala pema peponi roho za Marehemu wote, na awawezesha kupona haraka majeruhi 78 wa ajali hiyo, ili warejee katika hali ya kawaida na kuungana tena na ndugu na jamaa zao.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
9 Agosti, 2012

0 comments: