Subscribe:

search

.

Wednesday 15 August 2012

WASAFIRISHAJI WA WAHAMIAJI HARAMU KUSAKWA KILIMANJARO


Rehema Matowo, Rombo
MKOA wa Kilimanjaro unachunguza mtandao wa watu wanaopitisha wahamiaji haramu kinyume cha sheria.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama alisema suala la uhamiaji haramu limekuwa tatizo kubwa mkoani hapa na kwamba, kuna mtandao wa watu wanajihusisha na biashara ya kuwasafirisha kutoka Kenya.
“Watu hawawezi kupita tu bila kuwa na watu wanaowaongoza, tunachokifanya ni kuchunguza mtandao mzima na tumekubaliana kuwa, tutakuwa na kikao Agosti 17, ambacho tutajadili na kuona njia ya kumaliza tatizo hili ambalo linatoa sifa mbaya kwa mkoa wetu,” alisema.
Gama alisema tayari wamepewa majina ya baadhi ya watu wanaojihusisha na biashara hiyo, hivi sasa wanafanya uchunguzi na ukiwabaini wahusika wanajihusisha na biashara hiyo hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.
Kuhusu suala la watumishi wa umma hususan polisi wanaolalamikiwa kujihusiha na mtandao wa kusafirisha wahamiaji hao, Gama alisema Serikali haitamvumilia mtumishi yeyote atakayebainika kujihusisha na biashara hiyo, huku akiwataka wananchi kutoa taarifa za siri.
Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Kilimanjaro, Amir Ally alisema sheria haina makali juu ya wahamiaji haramu wanaoingia nchini, ndiyo maana wakiwakamata wamekuwa wakiwarudisha kwao kuondoa usumbufu, kwani gharama za kuwalisha na kuendesha kesi mahakamani ni kubwa kuliko adhabu watakayopewa.
Ally alisema kati ya Januari na Juni mwaka huu, zaidi ya wahamiaji haramu 600 wamekamatwa mkoani hapa wakiwa safarini kuelekea Afrika Kusini na kwamba, mtandao ni mkubwa kuanzia ngazi ya kijiji hadi serikali kuu na biashara hiyo itakoma pindi wananchi watakapokuwa tayari kuwataja mawakala.
Chanzo:Mwananchi.co.tz

0 comments: