Subscribe:

search

.

Friday 12 October 2012

ALICHOAMUA MH.MNYIKA HIKI HAPA


NIMECHUKUA HATUA YA KUWASILISHA KWA TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA SUALA LA MATATIZO YA MAJI KATIKA KATA YA GOBA ILI HATUA ZA HARAKA NA ZA KUDUMU ZICHUKULIWE

Kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi, kushiriki katika kutunga sheria na kuisimamia serikali ili kuwezesha maendeleo kwa pamoja na mambo mengine kuhakikisha huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji zinaboreshwa.
Tarehe 10 Oktoba 2012 ikiwa ni sehemu ya kufanya kazi hiyo nimekwenda kwa niaba ya wananchi Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na kuwasilisha malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu za kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora katika uendeshaji wa miradi ya maji kwenye kata ya Goba katika Manispaa ya Kinondoni.

Tatizo la maji katika kata ya Goba limedumu sasa kwa kipindi cha miaka mingi kabla ya mimi kuchaguliwa kuwa mbunge, pamoja na kwamba serikali inaowajibu wa kuhakikisha inalinda haki ya kupata maji lakini Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imeshindwa kulinda haki hii kwa wakazi wa Goba.

Ifahamike kuwa miongoni mwa haki za kijamii kwa mujibu wa Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kiutamaduni (“The International Covenant on Economic, Social and Cultural Rights”, ICESCR ) wa 1966 ni pamoja na haki ya kupata maji safi na salama.

Hata hivyo katika nchi yetu inaonekana haki ya kupata maji safi na salama haitiliwi mkazo pamoja na Tanzania kutambua na kuridhia mkataba huo hivyo malalamiko haya ya lengo la kuwezesha tume kusimamia haki za msingi za binadamu na utawala bora katika sekta ya maji.
Ikumbukwe kuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, toleo la mwaka 2005 Ibara ya 130 (b) na (c) inaeleza majukumu ya Tume ya Haki za binadamu na utawala bora kuwa ni pamoja na kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu na kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa utawala bora;
Izingatiwe kuwa Sheria ya Haki za binadamu na Utawala Bora namba 7 ya mwaka 2001 kifungu cha 22(1) kinaruhusu malalamiko kwa njia ya maandishi ;
Na Irejewe kuwa kuwa kifungu cha 15(1) (b) (iii) cha Sheria ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, sheria namba 7 ya mwaka 2001, kinaipa nguvu Tume kuchunguza uvunjaji wa Haki za Binadamu ikiwa itapokea malalamiko kutoka kwa mtu anayefanya hivyo kwa niaba ya kundi la watu.

Kwa kutumia mamlaka na matakwa ya Ibara ya 130 ya Katiba ya Nchi na vifungu vya 15 na 22 vya Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na utawala bora na kwa kuzingatia mikataba ya haki za binadamu ambayo nchi yetu imeridhia nimetaka tume ichukue hatua zifuatazo:

Mosi; Ichunguze na kuchukua hatua dhidi ya waliohusika katika ukiukwaji wa haki za binadamu za wananchi kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora kwa kushindwa kushughulikia matatizo ya kimfumo kuhusu uendeshaji wa miradi ya maji, kutokutekelezwa kwa wakati kwa vipaumbele vya maji kwa mujibu wa bajeti iliyopitishwa na tuhuma za ufisadi, uzembe na udhaifu wa kiutendaji katika kamati za maji, ngazi ya kata na kwenye idara ya maji ya Manispaa ya Kinondoni.


Pili; Pamoja na kuchukua hatua kwa wahusika waliosababisha uvunjaji wa haki ya msingi ya wananchi kupata huduma ya maji na ukiukwaji wa haki za binadamu; Tume ya Haki za Binadamu ipendekeze hatua za haraka zinazopaswa kuchukuliwa na Manispaa ya Kinondoni kuwezesha huduma ya maji kurejea kwa wananchi, kupanua kwa dharura wigo wa upatikanaji wa maji kwa wananchi wa Kata ya Goba pamoja na kuboresha mfumo mzima wa upangaji, utekelezaji na usimamizi wa miradi ya maji katika Manispaa ya Kinondoni.


Tatu; Aidha, zaidi ya hatua za dharura Tume ya Haki za Binadamu ipendekeze hatua za ziada ya kuchuliwa na Manispaa ya Kinondoni kuwezesha kata ya Goba itoke katika kupatiwa huduma ya maji chini ya Manispaa ya Kinondoni na badala yake ihudumiwe na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASA) pamoja na Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) ili kuwezesha uboreshaji mpana wa miundombinu kwa ajili ya ufumbuzi wa kudumu.
Nne, Tume ichunguze na kupendekeza masuala mengine ya kushughulikiwa na mamlaka zingine zinazohusika ikiwemo Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Wizara ya Maji na Vyombo vya Ulinzi na Usalama kuhusu masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu na uvunjwaji wa misingi ya utawala bora katika miradi ya maji kwenye kata ya Goba pamoja mfumo wa upatikanaji wa maji kwa ujumla.

Wenu katika kuwakilisha wananchi,


John Mnyika (Mb)

12/10/2012

0 comments: